1. Jinsi Mungu Anavyozungumza Nasi Kupitia Katika Biblia
"Mwanaume
yule na mkewe wakasikia sauti ya BWANA Mungu alipokuwa akitembea mle
bustanini wakati wa jua kupunga, nao WAKAJIFICHA ASIWAONE BWANA MUNGU
katikati ya miti ya bustani." (Mwanza 3:8).
Dhambi ilikata
mawasiliano ya ana kwa ana kati ya mwanadamu na Mungu. Baada ya dhambi
kuingia katika ulimwengu huu, je, Mungu aliwasilianaje na watu?
"Hakika Bwana Mwenyezi hafanyi kitu, bila kuwafunulia watumishi wake manabii nia yake." - Amosi 3:7.
Mungu hakutuacha sisi gizani kuhusu maisha haya tuliyo nayo na maana
yake. Kupitia kwa manabii wake - yaani, watu wale aliowaita Mungu kuwa
wanenaji na waandishi wake - wamefunua majibu yake kwa maswali makuu
yahusuyo maisha yetu.
2. Ni Nani Aliyeiandika Biblia?
Manabii waliutoa ujumbe wa Mungu kwa kutumia sauti na kalamu zao katika
kipindi chao walichoishi, na walipokufa, maandiko yao yaliendelea kuwapo
baada yao. Kisha ujumbe huo wa manabii ulikusanywa pamoja chini ya
uongozi wake Mungu, na kuwekwa katika kitabu tunachokiita Biblia.
Lakini maandiko yao hayo yanaaminika kwa kiasi gani?
"Zaidi ya hayo, lakini kumbukeni kwamba hakuna mtu ye yote awezaye
kufafanua mwenyewe unabii ulio katika Maandiko Matakatifu. Maana hakuna
ujumbe wa kiunabii unaotokana na matakwa ya binadamu bali watu walitoa
unabii wakiongozwa na Roho Mtakatifu" (2 Petro 1:20,21).
Waandishi wa Biblia waliandika si kwa kufuata mapenzi au tamaa yao, bali
kama walivyoongozwa au kuvuviwa na Roho wa Mungu. Biblia ni kitabu cha
Mungu!
Katika Biblia hiyo Mungu hutuambia habari zake Mwenyewe,
tena hutufunulia makusudi yake aliyo nayo kwa ajili ya wanadamu.
Inaonyesha mtazamo wa Mungu kwa mambo yale yaliyopita, kisha
inatufunulia mambo ya mbele, ikitueleza jinsi tatizo la uovu
litakavyotatuliwa mwishoni na jinsi amani itakavyokuja katika dunia
yetu.
Je, hivi Biblia yote ni ujumbe utokao kwa Mungu?
"Maandiko yote, Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa
kuonya, kusahihisha makosa yao, na kuwaongoza, katika kufundishia
ukweli, mtu wa Mungu awe mkamilifu na tayari kabisa kufanya kila kazi
njema, waishi maisha adilifu" - (2 Timotheo 3:16,17).
Biblia
Takatifu huyabadilisha kabisa maisha ya wanadamu kwa sababu Biblia
"yote" ina "pumzi ya Mungu," ni hati iliyovuviwa, ni kitabu cha Mungu.
Manabii walisimulia kile walichokiona na kukisikia kwa kutumia lugha ya
wanadamu, lakini ujumbe wao ulitoka moja kwa moja kwa Mungu. Kwa hiyo,
ukitaka kujua maisha haya yana maana gani, soma Maandiko Matakatifu.
Kuisoma Biblia kutayabadilisha kabisa maisha yako. Kadiri unavyozidi
kuisoma kwa maombi, ndivyo utakavyozidi kupata amani moyoni mwako.
Roho Mtakatifu yule yule aliyewavuvia manabii kuandika, Biblia hiyo,
atayafanya mafundisho ya Biblia, injili yake, ifae kuyabadilisha kabisa
maisha yako ukimwalika Roho kuwapo wakati unapoisoma hiyo Biblia.
3. Umoja wa Biblia
Kwa kweli Biblia ni maktaba ya vitabu 66. vitabu 39 vya Agano la Kale
viliandikwa kuanzia karibu na mwaka wa 1450 K.K hadi 400 K.K, Vitabu 27
vya Agano Jipya viliandikwa kati ya mwaka wa 50 B.K na mwaka wa 100 B.K.
Nabii Musa alianza kuandika vitabu vitano vya kwanza wakati fulani
kabla ya mwaka wa 1400 K.K. Mtume Yohana alikiandika kitabu cha mwisho
cha Biblia, yaani, kitabu cha Ufunuo, karibu na mwaka wa 95 B.K. Katika
kipindi cha miaka 1,500 kati ya kuandikwa kitabu cha kwanza na cha
mwisho cha Biblia, walau watu wengine wapatao 38 waliovuviwa walitoa
mchango wao. Wengine walikuwa wafanya biashara, wengine wachungaji wa
kondoo, wengine wavuvi, wengine askari, matabibu, wahubiri, wafalme -
wanadamu toka katika tabaka zote za maisha. Mara nyingi waliishi katika
utamaduni na falsafa vilivyohitilafiana.
Lakini hapa ndipo yalipo
maajabu ya maajabu yote: Vitabu hivyo 66 vya Biblia pamoja na sura zake
1,189 zenye idadi ya mafungu 31,173 vikiwekwa pamoja, tunaona umoja na
mwafaka katika ujumbe vinavyoutoa
4. Waweza Kuiamini Biblia
a). Kuhifadhiwa kwa Biblia ni jambo la ajabu sana. Maandiko yote ya
awali ya Biblia yalinukuliwa kwa mkono - muda mrefu kabla ya kuwako
mitambo ya kuchapisha vitabu. Waandishi wale walitayarisha nakala za maandiko ya mkono ya asilia na kuzitawanya.
Maelfu ya nakala kama hizo za maandiko ya mkono au sehemu zake bado ziko mpaka sasa.
Maandiko ya mkono ya Kiebrania yanayorudi nyuma hadi ule mwaka wa 150
mpaka 200 kabla ya Kristo yalipatikana karibu na Bahari ya Chumvi mnamo
mwaka 1947. Ni jambo la kushangaza sana kwamba magombo hayo mawili yenye
umri wa miaka elfu mbili yanazo kweli zile zile tunazozikuta katika
Agano la Kale la Biblia zinazochapishwa siku hizi. Huu ni ushahidi wenye
nguvu unaoonyesha jinsi Neno la Mungu linavyoaminika.
Mitume
waliandika kwanza sehemu kubwa ya Agano Jipya kama nyaraka walizozituma
kwa makanisa ya Kikristo yaliyoanzishwa baada ya kifo na ufufuo wake
Kristo. Zaidi ya maandiko ya mkono 4,500 ya Agano Jipya lote au sehemu
yake yanapatikana katika nyumba za Makumbusho na maktaba za Ulaya na
Amerika. Baadhi yake yanakwenda nyuma hadi karne ile ya pili.
Kuyalinganisha maandiko hayo ya mkono ya awali na biblia ya siku hizi,
twaweza kuona kwa urahisi kwamba kwa kawaida Agano Jipya limeendelea pia
kubaki bila mabadiliko yo yote tangu lilipoandikwa kwa mara ya kwanza.
Siku hizi Biblia au sehemu zake zimetafsiriwa katika lugha zaidi ya
2,060 . Ni kitabu kinachouzwa sana ulimwengu: zaidi ya Biblia milioni
150 na sehemu za Biblia huuzwa kila mwaka.
a). Usahihi wa Biblia
kihistoria ni wa kushangaza sana. Uvumbuzi mwingi wa elimu ya mambo ya
kale (akiolojia) umethibitisha kwa namna ya kuvutia sana usahihi wa
Biblia. Wanahistoria wamevigundua vibao vya udongo wa mfinyanzi pamoja
na majengo ya kumbukumbu ya mawe ambayo yameonyesha majina, mahali, na
matukio yaliyojulikana kuhusu siku za nyuma kutokana na Biblia tu.
c) Kutimia kwa usahihi kabisa kwa utabiri wa Biblia hukuonyesha wewe
kwamba unaweza kuitegemea Biblia. Maandiko hayo yana utabiri mwingi wa
kushangaza sana wa matukio ya siku za usomi ambayo hivi sasa yanaendelea
kutimia mbele ya macho yetu.
5. Jinsi Ya Kuielewa Biblia
Unapolichunguza Neno la Mungu, weka kanuni hizi mawazoni mwako:
A). Jifunze Biblia ukiwa na moyo wa maombi. Ukiyaendea Maandiko
Matakatifu kwa moyo na mawazo yaliyofunguliwa kwa maombi, yatageuka na
kuwa mawasiliano kati yako na Yesu (Yohana 16:13-14).
B). Soma
Biblia kila siku. Kujifunza Biblia kila siku ni ufunguo wa kupata nguvu
katika maisha yetu, ni kukutana na mawazo ya Mungu (Warumi 1:16).
C) Unapoisoma, iache Biblia ijieleze yenyewe. Uliza: mwandishi huyu wa
Biblia alikusudia kusema nini? Kwa kuzingatia kile limaanishacho fungu
hilo, twaweza kuitumia kwa akili katika maisha yetu ya leo hii.
D) Soma Biblia kwa kufuata somo. Linganisha andiko na andiko. Yesu
alitumia mbinu hii kuthibitisha kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi:
"Akaanza kutoka Musa na Manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe."
E)Jifunze Biblia ili kupokea uwezo wa kuishi kwa ajili ya Kristo. Neno
la Mungu limeelezwa katika Waebrania 4:12 kama upanga mkali ukatao
kuwili. Ni zaidi ya maneno tu yaliyo juu ya ukurasa, ni silaha iliyo hai
mikononi mwetu ya kupigia na kuyaondolea mbali majaribu yale
yanayotushawishi kutenda dhambi.
F).Sikiliza Mungu anapozungumza
nawe kupitia katika Neno lake. Endapo mtu anataka kuujua ukweli wa
Bilbia juu ya somo fulani, basi, ni lazima awe tayari kufuata yale
inayofundisha (Yohana 7:17), sio yale anayofikiri mtu fulani, au yale
yanayokaziwa na fundisho lolote la kanisa lake.
G). Biblia Yaweza
Kubadilisha Maisha Yako.."Kuyafafanua maneno yako [Mungu] kwatia nuru,
kunampa ufahamu mjinga" - (Zaburi 119:130).
Kujifunza Biblia
kutauimarisha "ufahamu" wako, kutakupa nguvu ya kuyashinda mazoea yale
yaletayo madhara, na kukuwezesha kukua kimwili, kiakili, kimaadili na
kiroho.
Biblia inazungumza na moyo. Inashughulika na mambo yale
yanayowapata wanadamu katika maisha yao - yaani, upendo, ndoa, uzazi na
kifo. Inaliponya jeraha lenye kina kirefu sana katika tabia ya
mwanadamu, pamoja na dhambi na taabu inayotokana nayo.
Neno la
Mungu si kitabu cha jamii moja, kizazi kimoja, taifa moja, au utamaduni
mmoja. Japokuwa liliandikwa katika nchi ya Masharikiya kati, linawavutia
pia wanaume na wanawake wa Magharibi. Linaingia katika nyumba za
wanyonge na katika majumba makubwa ya matajiri. Watoto wanazipenda
hadithi zake zinazosisimua. Mashujaa wake wanawavutia sana vijana.
Wagonjwa, wanaoishi katika hali ya upweke, na wazee wanagundua ndani
yake faraja na tumaini la kuwa na maisha bora.
Neno la Mungu
[Biblia[ Inaivunjavunja hata mioyo iliyofanywa migumu dhidi ya hisia
zote za kibinadamu, inailainisha na kuijaza na upendo.
👉Tumeona Biblia ikimbadilisha haramia wa zamani na mvuta bangi na kumfanya mhubiri aliye motomoto.
👉Tumeona Biblia ikimbadilisha mwongo na mdanganyaji na kumfanya kuwa mwalimu mwaminifu na mwenye kuheshimika.
👉 Tumeona kitabu hicho kikiwanyakua watu wakiwa karibu na kujiua wenyewe na kuwapa tumaini la kuanza maisha upya.
👉 Biblia inaamsha upendo miongoni mwa maadui. Inawafanya wenye majivuno kuwa wanyenyekevu, na wachoyo kuwa wakarimu.
👉Biblia
inatutia nguvu tunapokuwa dhaifu, inatuchangamsha tunapokuwa katika
hali ya kukata tamaa, inatufariji tunapokuwa na huzuni, inatuongoza
tunapochoka sana. Inatuonyesha jinsi ya kuishi kwa ujasiri na jinsi ya
kufa bila hofu.
Mtu mmoja alishuhudia akiwa gerezani ...."Mimi
nimo gerezani, niko katika orodha ya watu wanaostahili kunyongwa,
nimehukumiwa kufa kwa kutenda kosa la jinai. Kabla ya kuchukua kozi hii
ya Biblia, nilikuwa nimepotea lakini sasa ninacho kitu cha kutumainia
tena nimeupata upendo mpya."
👉Kitabu
hicho cha Mungu, yaani, Biblia kinaweza kuyabadili maisha yako pia
"Lakini hizi [kweli za Biblia] zimeandikwa; ili mpate kuamini ya kwamba
Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini muwe na uzima ..
tunapaswa kuyafahamu Maandiko Matakatifu ni kwa sababu yamejaa picha
zinazomfunua Yesu Kristo na kutuhakikishia sisi uzima wa milele. Kwa
kumtazama Kristo katika Biblia nzima, tunabadilika na kufanana naye
zaidi.
Biblia inao uwezo unaoweza kuyabadilisha kabisa maisha ya
watu. Kwa kweli, watu wanapoanza kujifunza Biblia, maisha yao hubadilika
kwa namna ya kuvutia sana.